Wednesday 24 January 2018

HADITHI!!!......SEHEMU YA SITA

BIASHARA YA KIFO
Sehemu ya 06


Maisha yaliendelea kama kawaida. Hakukuwa na kitu kilichokisumbua kichwa cha padri Benedicto kama kumuona mzazi mwenzake akiishi mbali naye. Hakuwa na uwezo wa kwenda kukaa naye lakini kila siku alikuwa mtu wa kutamani kumuona mwanamke huyo akiwa karibu naye kwani ndiye mtu pekee aliyeonekana kuwa faraja katika maisha yake.
Kutokana na mapenzi mazito aliyokuwa nayo juu yake, muda wote alihisi kwamba alikuwa akiibiwa tu. Aliwafahamu vijana wa Sinza, walikuwa vijana makini kuhusu masuala yote ya mapenzi, walikuwa na uwezo mkubwa wa kumteka msichana yeyote hata kama angekuwa mgumu kiasi gani.
Hakutaka kusalitiwa, alitaka Irakoze awe wake peke yake, hivyo alichokifanya ni kuanza kupanga mipango kabambe ya kumbana mwanamke huyo kwa kumpeleka katika Chuo cha Utawa,  St. Mary’s Catholic kilichokuwa Gongo la Mboto jijini Dar es Salaam na kuingia pale kama mpishi.
Mipango yote ya Irakoze kuingia ndani ya chuo kile ilifanywa na padri Benedicto huku akimchukua Annabel na kumpeleka nchini Marekani kwa ajili ya kusoma huko katika Shule ya Consolatha Seminary School iliyokuwa katika Jiji la New York nchini Marekani.
Kidogo moyo wake ukawa na amani, kutokana na umbo lake kuwa dogo na sura ya kitoto aliyokuwa nayo, mara baada ya kufika katika chuo hicho cha Utawa, masista wote walihisi kwamba Irakoze alikuwa msichana mdogo, hivyo wakamchukulia hivyohivyo.
Kila siku alikuwa hapo huku akiwasiliana na padri Benedicto simuni, bado wawili hao waliendelea kuwa kwenye mahusiano ya kimapenzi kwa siri sana kiasi kwamba hakukuwa na mtu yeyote aliyefahamu kilichokuwa kikiendelea.
Huo ulikuwa mwaka wake wa kwanza chuoni hapo, alionekana kuwa mtu mwenye heshima, alimheshimu kila mtu kuanzia wale wa chini mpaka wa juu. Wasichana wengi waliokuwa chuoni hapo walimpenda Irakoze ambaye walipenda kumuita kwa jina la Sista Magdalena.
Siku zikaendelea kukatika, kila alipokuwa akitumwa mjini kwa ajili ya kununua baadhi ya vitu kwa ajili ya shule hiyo, alikuwa akienda na kuonana na padri Benedicto na kisha kulala wote hata kwa masaa mawili kisha kurudi chuoni.
Huko ndipo alipopata taarifa kuhusu binti yake aliyekuwa nchini Marekani. Masomo yaliendelea vizuri na mara kwa mara safari za Benedicto kuelekea nchini Marekani hazikuisha, kila alipokwenda, alihakikisha anaonana na binti yake na kisha kurudi nchini Tanzania.
“Amekua sana, mwaka wa sita huu,” alisema Benedicto, alikuwa akimwambia Irakoze.
“Nina kiu ya kumuona.”
“Usijali! Ila nataka tuifanye kitu kimoja”
“Kipi?”
“Na wewe usomee utawa!”
“Mmmh!”
“Hakuna tatizo! Utafanikiwa tu, nataka uwe na safari za kutosha kwenda Ulaya na sehemu nyingine,” alisema Benedicto.
“Sawa! Hakuna tatizo!”
Hilo ndilo walilokuwa wamekubaliana, ilikuwa ni lazima Irakoze aanze kusomea utawa ndani ya chuo hicho alichokuwa akifanya kazi kama mpishi. Hilo wala halikuwa tatizo, kwa sababu tayari alikwishafanya kazi hiyo kwa miaka mitatu, akachukuliwa na kuanza masomo moja kwa moja.
Kila siku alikuwa akiamka asubuhi na mapema kama wanachuo wengine na kisha kuelekea kanisani ambapo walisali kisha kujiandaa na masomo kama kawaida. Japokuwa hakuwa amesoma sana kipindi cha nyuma lakini uwezo wake wa kawaida ulitosha kabisa kuonyesha kwamba kama angeendelea zaidi basi angeweza kufanikiwa sana katika maisha yake.
Aliishi kama mtumishi wa Mungu, kila wakati alikuwa mtu wa kusali huku rozali ikiwa shingoni mwake. Kila mtu alimheshimu na alipoonekana kwamba yeye ndiye alikuwa mcha Mungu mkubwa kuliko wengine, wakampa uongozi wa bweni pasipo kujua kwamba mwanamke huyo alikuwa na mtoto ambaye alikuwa akisoma nchini Marekani.
Padri Benedicto hakuacha, kwa kuwa katika kila hatua aliyokuwa akipitia Irakoze ilikuwa chini yake, hivyo alihakikisha kwamba hata kwenda nje ya chuo hicho linakuwa jambo jepesi ili mradi mwisho wa siku aweze kuonana naye na kufanya mambo yao.
Alichokifanya ni kukaa chumbani na kuandika barua, alikuwa akiuandikia uongozi wa chuo hicho kwamba kutokana na heshima aliyokuwa nayo Irakoze, aliruhusiwa kila Jumapili kwenda kusali nje ya chuo hicho.
Nafasi hiyo haikutolewa mara kwa mara, ilitolewa mara chache sana tena kwa wanachuo walioonekana kuwa na nidhamu ya hali ya juu. Kwa Irakoze hakukuwa na mtu aliyeonekana kuwa na wasiwasi, jinsi nidhamu yake ilivyokuwa chuoni hapo, ilimfanya kila mmoja kukubaliana na padri Benedicto kutokana na jinsi alivyokuwa chuoni hapo.
Hiyo ndiyo ilikuwa nafasi nyingine na waliitumia vilivyo kuwa pamoja. Kila kitu kilichokuwa kikifanyika kiliendelea kuwa siri kubwa. Baada ya miaka miwili kukatika, hatimaye aliyekuwa Kardinari wa Kanisa la Kiroma nchini Tanzania, Paulo Alonso akafariki dunia na hatimaye barua kuandikwa kutoka Vatican kwamba Padri Benedicto alitakiwa kutawazwa na kuchukua nafasi hiyo kwani kwa sifa zote za kuwa kardinari alikuwa nazo.
“Lakini kwa nini apewe padri? Kwa nini asipewe askofu?” maaskofu waliulizana tu.
“Hata sisi hatufahamu, ila kwa sababu ni barua iliyoletwa kutoka Vatican, hatuna budi, acha tukubaliane nayo,” alisema askofu mmoja.
Baada ya wiki mbili, padri Benedicto alitakiwa kuelekea nchini Vatican kwa ajili ya kutawazwa na hatimaye kuwa kardinari mkubwa nchini Tanzania. Hiyo ilikuwa nafasi yake pekee, moyo wake ulikuwa na furaha kubwa, hakukuwa na kitu kilichowahi kumpa furaha maishani mwake kama kipindi hicho.
Suala la kuwa na mtoto liliendelea kuwa siri yake, hakutaka mtu yeyote afahamu na alikuwa akijitahidi kufanya kila liwezekanalo kusiwe na mtu yeyote anayelifahamu hilo. Kwenye kila mwaka, alikuwa akimtumia mtoto wake Annabel kiasi cha fedha kwa kutumia akaunti nyingine kabisa iliyosomeka kwa jina la Andrew McDonald, raia kutoka nchini Kenya.
Japokuwa Annabel katika kipindi hicho alikuwa na miaka kumi, lakini aliendelea kufichwa kwamba baba yake alikuwa padri ambaye katika kipindi hicho alitarajiwa kutawazwa na kuwa kardinari nchini Tanzania.
“Unataka kuwa nani ukikua?” aliuliza Benedicto.
“Nataka kuwa mwanasheria.”
“Kwa nini usiwe sista?”
“Sitaki! Nitataka niolewe. Nimesikia kwamba sista haolewi! Kweli baba?”
“Ndiyo!”
“Basi mimi nataka kuwa mwanasheria, ninataka kuolewa baadaye!”
Alikuwa akizungumza na binti yake katika kipindi alichokwenda kumtembelea nchini Marekani. Japokuwa alikuwa nchi nyingine lakini kofia aliyokuwa ameivaa haikutoka kichwani mwake. Shule hiyo aliyompeleka binti yake kusoma ilimtunza vizuri, alipata malezi yote na hakukuwa na shida sana kwa kuwa mara kwa mara alikuwa akifika hapo na kumuona.
Annabel alikuwa binti mzuri, mwenye sifa zote za kuitwa mrembo. Alichanganyikana, alikuwa na sura ya baba yake lakini pia alikuwa na sura ya mama yake. Watu wengi waliokuwa wakimuona, walikiri kwamba binti huyo angekuja kutikisa sana siku za usoni kutokana na urembo wake huo.
“Baba!”
“Naam!”
“Unafanya kazi gani?”
“Mimi?”
“Ndiyo!”
“Kwani sijawahi kukwambia binti yangu?”
“Hapana! Hukuniambia!”
“Mimi ni mfanyabiashara binti yangu, huwa nasafirisafiri sana,” alijibu Benedicto.
“Kweli baba?”
“Ndiyo! Nikitoka hapa, nakwenda Dubai, nikuletee zawazi gani nikija?”
“Chochote upendacho baba, nitafurahi!” alisema Annabel.
Benedicto hakuwa na jinsi, ni kweli alimpenda binti yake lakini kulikuwa na vitu ambavyo hakutakiwa kuwa mkweli kabisa, alimdanganya kwamba alikuwa mfanyabishara kwa kuwa hakutaka ajue kwamba alikuwa padri ambaye hakutakiwa kuoa au kuwa na mtoto yeyote yule.
Kwake, bado lile liliendelea kuwa siri kubwa, kila siku lilimuumiza moyoni mwake lakini hakuwa na jinsi, alikubaliana na kila kitu kilichokuwa kiiendelea, na hata kama alifanya dhambi, aliamini kwamba hakukuwa na mwanadamu aliyekuwa mkamilifu mbele za Mungu.
Baada ya siku tatu, akarudi nchini Tanzania ambapo moja kwa moja akawasiliana na Irakoze na kumwambia kuhusu mtoto wao na ndoto aliyotaka kuwa nayo katika maisha yake.
“Kakataa kuwa sista?”
“Amekataa!”
“Daaah! Ngoja niende, nitazungumza naye,” alisema Irakoze.
“Hakuna tatizo!”
Japokuwa aliamini kwamba binti yake angeweza kumsikiliza na hatimaye kukubaliana nao kuwa sista lakini hilo halikuwezekana, bado msimamo wa Annabel ulikuwa ni kuwa mwanasheria mkubwa duniani.
Hakukuwa na mtu aliyemzuia, waliachana naye, aendelee na maisha yake na mwisho wa siku kukamilisha kile alichokuwa akikitaka.
Wakati Annabel akifikisha miaka kumi na sita, alionekana kuwa binti mrembo mno, kipindi kirefu cha maisha yake alikitumia nchini Marekani, hakuwahi kurudi nchini Tanzania, aliondoka huko miaka mingi iliyopita, tangu alipokuwa na miaka minne.
Hakufahamu sehemu yoyote nchini Tanzania, hakufahamu mitaa na hata watu wa huko walikuwa na utamaduni gani. Baada ya kufikisha miaka hiyo, hakutaka kukaa nchini Marekani, alitaka kuwa na muda wa kurudi nchini Tanzania ili aweze kukaa na wazazi wake ambao hakuwahi kukaa nao hata siku moja.
Alitaka malezi yao, alichokifanya ni kuwasiliana nao, hawakuwa najinsi, wakajipanga kwamba mara binti yao atakapofika nchini Tanzania, wampelekea katika nyumba yao nyingine iliyokuwa Kisarawe, pembezoni mwa Jiji la Dar es Salaam ambapo waliamini kwamba hakukuwa na watu wengi.
Siku ya safari ilipofika, Annabel akaingia ndani ya ndege tayari kwa kurudi nchini Tanzania. Hapo Marekani akapanda ndege ya Shirika la Ndege la American Airlines ambayo ilikuwa ikifanya safari mpaka nchini Uingereza, Italia na baadaye kuelekea Uholanzi ambapo huko wangebadilisha ndege na kuelekea Dubai, kisha India na Kenya jijini Nairobi na kuingia nchini Tanzania kabla ya kuelekea Afrika Kusini.
Baada ya abiria kutakiwa kuingia ndani ya ndege hiyo, Annabel akasimama na kuanza kuelekea ndani ya ndege hiyo. Kwa muonekano, alionekana kuwa binti mkubwa, mrembo, mwenye mvuto ambaye alivutia sana, kila mwanaume aliyemwangalia, alitamani kuwa na msichana mrembo kama alivyokuwa.
Wakati ameingia ndani ya ndege hiyo na kukaa katika viti vya watu wawili, akaja mwanaume mmoja, alionekana kuwa kijana mtanashati, aliyependeza, alivalia suti ya gharama, muda wote uso wake ulionekana kuwa na tabasamu pana, alimuona Annabel, tabasamu likaongezeka usoni mwake.
“How are you cute,” (Habari yako, mrembo) alimsalimia Annabel.
“I’m fine, you are welcome,” (Salama, karibu) alimkaribisha mwanaume yule aliyejitambulisha kwa jina la Ethan Dylan.

INAENDELEA...                        

No comments:

Post a Comment