Sunday 21 January 2018

HADITHI!!!!!.........SEHEMU YA PILI

BIASHARA YA KIFO

Sehemu ya 02

Hawakujua kitu kilichokuwa kikiendelea nje, hawakujua kama kundi la wanawake likiongozwa na mama mwenye nyumba liliingia ndani na kukisogelea chumba walichokuwa huku wakiwa wamelaliana kimahaba.
Ghafla, huku wakiwa wametekwa na uwepo wa mahaba mahali hapo, wakashtukia mlango ukifunguliwa na kundi zima la wanawake hao kuingia ndani. Kwanza wakashtuka, wakawaangalia vizuri wanawake wale, alikuwepo mke wake pia.
Mzee Saidi akashtuka, hakuamini kile alichokuwa kikiona, mdomo wake ukawa mzito kusema chochote kile. Mkewe alionekana kuvimba kwa hasira, hakuamini kile alichokuwa akikiona chumbani humo, mume wake ambaye kila siku alikuwa akimuamini ndiye yule aliyekuwa na mwanamke kitandani kwake, tena mfanyakazi wake aliyemtoa kijijini.
Irakoze alivyoona hivyo, akaanza kuomba msamaha huku machozi yakimbubujika mashavuni mwake. Hata kabla bi Hadija hajazungumza lolote lile, akamvamia msichana huyo wa kazi na kuanza kumpiga.
Kundi lile la wanawake halikugobelezea, lilikuwa likishadadia kile kilichokuwa kikiendelea chumbani pale. Ni mzee Saidi ndiye aliyechukua jukumu la kuanza kuamulia lakini bi Hadija hakushikika, alikuwa akitukana hovyo.
“Wewe malaya kweli unaamua kunichukulia mume wangu, tena unalala naye kitandani kwangu, sasa utanitambua,” alisema bi Hadija huku akimshambulia Irakoze.
“Hadija, hebu muache mtoto wa watu.”
“Unagombelezea? Malaya mkubwa wewe, unagombelezeaaaaa?” 
Ugomvi ulikuwa mkubwa, wanawake wale wengine walikuwa wakizungumza maneno yenye kumuumiza Irakoze juu ya kile alichokuwa amekifanya, kila mmoja alimshutumu huku wengine wakimpiga masingi na kumzomea.
Irakoze aliumizwa kutokana na kipigo alichopewa lakini hakuwa na jinsi, kama maji, tayari yalikwishamwagika na hivyo kufukuzwa nyumbani hapo. Hakutakiwa kukaa, mchana huohuo akafukuzwa na kuondoka nyumbani hapo huku akilia, furushi la nguo zake lilikuwa mikononi mwake.
Alijutia kitendo alichokuwa amekifanya, alianza kujuta kwani kilimuumiza mno. Alipiga hatua kuelekea Magomeni Mikumi ambapo huko akachukua barabara ndogo iliyokuwa ikielekea Mwembe Chai kupitia ilipokuwa nyumba ya marehemu Sheikh Yahya.
Alipofika njiani, mvua kubwa ikaanza kunyesha, hakuwa na jinsi, alichokifanya ni kwenda kwenye nyumba moja aliyoiona kufaa na kisha kujikinga na mvua ile iliyokuwa ikinyesha mno. Hapo ndipo akachukua muda mwingi kuanza kulia, 
“Nitakwenda wapi mimi? Nitakwenda wapi mimi?” alijiuliza huku akilia.
Mvua ilichukua zaidi ya nusu saa mpaka kuacha kunyesha. Alipoona imeacha, hapo ndipo akalishika furushi la nguo zake na kisha kusonga mbele. Alikuwa akielekea wapi? Hakujua, alihitaji kuondoka mbali na nyumba ya mzee Saidi
 Alikwenda na barabara hiyo mpaka alipokuta njia panda, barabara moja ilikuwa ikielekea Mwembe Chai na nyingine Mburahati, alichokifanya ni kuchukua barabara ya kuelekea Mburahati ambapo aliamini kwamba angeweza kupata msaada wowote ule.
Alisonga mbele, furushi lilikuwa kichwani mwake huku akibubujikwa na machozi. Aliona dunia imemgeukia, hakuwa na pa kukimbilia zaidi ya kwenda mbele kama mtu aliyekuwa akibahatisha sehemu fulani.
Safari yake iliishia nje ya nyumba moja, haikuwa ya kifahari, ilikuwa nyumba ambayo kwa kiasi fulani ilionekana kuchoka. Kulijaa matope lakini hakutaka kujali, kwa kuwa kulikuwa na kibaraza, akaenda na kutulia hapo.
Kumbukumbu za maisha yake zikaanza kujirudia kama mkanda wa filamu kichwani mwake, alikumbuka mengi tangu siku ya kwanza alipofika jijini Dar es Salaam mpaka siku hiyo. Alihuzunika na kujutia uamuzi wake wa kutembea na mzee Saidi, ila pamoja na hayo yote, alitakiwa kupambana kwani alijua kwamba huo usingekuwa mwisho wa maisha yake.
“Habari yako!” ilisikika sauti ya mwanamke mmoja, alikuwa amefika nyumbani hapo huku mkononi akiwa ameshika Biblia.
“Salama! Shikamoo mama!”
“Marahaba binti mzuri, hujambo?”
“Sijambo!”
Baada ya salamu ile, mwanamke yule hakuongea kitu chochote kile zaidi ya kufungua mlango na kuingia ndani. Irakoze hakutoka kibarazani hapo, aliendelea kukaa huku akionekana kuwa na mawazo mengi.
Mpaka inafika saa kumi na mbili jioni, bado hakujua aende wapi, hakuijua vizuri Dar es Salaam kwani kipindi cha miaka miwili kukaa ndani ya jiji hilo, hakuwa mtembeaji, alikuwa mtu wa kutulia tu nyumbani, akitoka, kaenda gengeni na kurudi nyumbani.


INAENDELEA...

No comments:

Post a Comment