Wednesday 24 January 2018

HADITHI!!!!! HADITHI SEHEMU YA TANO

BIASHARA YA KIFO
sehemu ya 05

Kwa kumwangalia usoni tu, padri Benedicto alionekana kuhitaji msaada, alitia huruma mno, macho yake alikuwa ameyapeleka usoni mwa Irakoze huku akionekana kuwa na hofu kubwa. Kile alichokuwa amekifanya kilikuwa ni kinyume na sheria za kanisa hilo hivyo kama kanisa lingejua kile kilichokuwa kimetokea, lingekuwa tatizo kubwa.
Hakukuwa na mtu ambaye angeweza kumsaidia katika kipindi hicho zaidi ya msichana huyo. Alizungumza naye kwa kipindi kirefu, tena kwa unyenyekevu mkubwa na mwisho wa siku akamwambia ukweli kwamba alitakiwa kuondoka mahali hapo.
“Niende wapi?”
“Popote pale, ili mradi utoke ndani ya nyumba hii,” alisema padri Benedicto.
“Kwa hiyo unanifukuza?”
“Hapana! Sikufukuzi.”
“Ila?”
“Nitakupangia chumba, utakwenda kuishi huko mpaka utakapojifungua, nakuahidi kukusaidia kwa kila kitu,” alisema padri Benedicto.
“Una uhakika?”
“Ndiyo!”
Hicho ndicho walichokubaliana, padri hakutaka Irakoze abaki nyumbani hapo kwa kuhofia kwamba watu wangeweza kujua kwamba alikuwa mjauzito na hivyo mwisho wa siku kumletea matatizo, alichokifanya ni kumwambia aondoke nyumbani hapo huku akimgawia kiasi cha shilingi milioni moja.
Kabla ya kuondoka kwanza akaanza kutafuta chumba ambacho alikipata maeneo ya Sinza Makaburini, huko ndipo alipoanza maisha yake. Alikuwa akihudumiwa kila kitu na padri huyo, kuanzia chakula, mavazi, vitu vya ndani na mambo mengine mengi.
Alipewa kiasi cha shilingi milioni moja kila mwezi kitu kilichompeleka kuanza kufanya biashara zake binafsi, japokuwa zilikuwa ndogondogo lakini akafanikiwa kwa kiasi kikubwa kuyaendesha maisha yake.
Katika kipindi hicho cha kwanza tumbo lake halikuwa likionekana lakini baada ya miezi kadhaa kupita, kila mtu aliyekuwa akimwangalia alijua kwamba msichana huyo alikuwa mjauzito.
Padri Benedicto akawa akifika sana nyumbani hapo nyakati za usiku tena huku akiwa amevalia kofia kubwa ili asiweze kujulikana. Kila kitu kilichokuwa kikiendelea, kilikuwa siri kubwa mno kiasi kwamba hakukuwa na mtu aliyefahamu ukweli.
Baada ya miezi tisa kukatika, hatimaye Irakoze akajifungua mtoto wa kike aliyempa jina la Annabel kama ambavyo padri Benedicto alivyotaka aitwe na hivyo maisha yake na mtoto wake kuanza.
Padri huyo hakukata mguu nyumbani hapo, kila alipomuona Annabel, moyoni mwake alijisikia furaha mno, hakuamini kama mwisho wa siku na yeye alifanikiwa na kuitwa baba. Moyoni mwake alijiona kuwa mwanaume wa shoka, alijikubali japokuwa sheria ya kidini ilimkataza kuwa na mwanamke yeyote, kuona au kuzaa mtoto.
Siku zaikaendelea kukatika, hakuacha kufika nyumbani hapo, aliendelea kumlea Irakoze na mtoto wake na baada ya miaka mitatu kupita huku akiwa amekwishaanza kumjengea nyumba Irakoze maeneo ya Mbezi Beach, hapo ndipo alipoamua kumwanzisha Annabel Shule ya Chekechea ya Antonino iliyokuwa Mbezi Beach ambapo wanafunzi wengi walisoma shuleni hapo walikuwa ni wale waliotoka katika familia za kitajiri.
Mwaka uliofuata ambapo Annabel aliingia mwaka wa nne hapo ndipo alipoanza kumsumbua mama yake kuhusu baba yake. Kila siku alikuwa mtoto wa kulia tu, hakukuwa na kitu alichokuwa akikitamani wakati huo kama kumuona baba yake tu.
“Mama nataka kumuona baba.....” alisema Annabel kwa sauti ya chini huku akilia.
“Baba yako atakuja.”
“Lini?”
“Kesho! Twende shule kwanza.”
“Sitaki kwenda mpaka nimuone baba.”
“Atakuja tu mwanangu! Twende shule kwanza.”
Japokuwa aligoma kwenda shule lakini Irakoze hakuwa na jinsi, alimlazimisha Annabel mpaka akakubali kwenda shuleni. Njiani, alikuwa akilia tu, hakunyamaza, kila walipofika bado alikuwa akilia kumuona baba yake.
Hicho kilimuumiza sana Irakoze, kila aliposikia kwamba binti yae mzuri akimuulizia baba yake, moyo wake ulimuuma mno. Hakuwa na jinsi, alimpigia simu padri Benedicto na kumwambia ukweli kwamba binti yake alitaka kumuona, hivyo alitakiwa kufanya kila awezalo aje kumuona.
“Nitakuja.”
“Lini?”
“Sijajua! Ila nitakuja hivi karibuni.”
“Unajua mtoto wako anasumbua sana, siku hizi hata kula hataki!”
“Kisa?”
“Anataka kukuona wewe!”
“Aiseee! Nitakuja basi.”
“Lini?”
“Kesho usiku!”
“Sawa!”
Siku iliyofuata usiku, padri Benedisto alikuwa mahali hapo, kitu cha kwanza kabisa alitaka kumuona binti yake. Japokuwa mara kwa mara alikuwa akifika na kumuona lakini siku hiyo Irakoze akaamua kumwambia Annabel kwamba yule alikuwa baba yake.
Annabel akafuata na kumkumbatia, alionekana kuwa na furaha sana na hakutaka kutoka mikononi mwa baba yake. Kila alipomwangalia binti yake, alifanana naye sana, alijifariji sana, japokuwa sheria hazikutana padri kuwa na mtoto lakini kwake ilionekana kuwa furaha kubwa. 
Kuanzia siku hiyo, mara kwa mara alikuwa akifika nyumbani hapo huku akimkataza Irakoze asimwambie Annabel kama alikuwa padri kuepuka matatizo hapo baadae. Hilo wala halikuwa tatizo, Irakoze akakubaliana naye kwamba jambo hilo liendelee kuwa siri siku zote.

“I will kill you, bullshit,” (Nitakuua kinyesi cha ng’ombe)
“Do you really want to kill me?” (Unataka kuniua?)
“Yes!” (Ndiyo!)
“Ok! Just shoot me.” (Sawa! Nipige risasi)
“I will kill you.” (Nitakuua)
“Shoot me! Shoot me right here,” (Nipige risasi, nipige hapa)
Lilikuwa kundi kubwa la watu zaidi ya thelathini waliozunguka sehemu iliyokuwa na mapipa makubwa ya uchafu katika mtaa wa kimasikini wa Manhattan uliokuwa katika Jiji la New York nchini Marekani.
Kila mtu alikuwa akimwangalia kijana aliyeshika bunduki, alikuwa amemnyooshea mwanaume mmoja, alionekana kuwa mtu mzima, alikuwa akitamka maneno kwamba angempiga na risasi endapo tu angeendelea kuzungumza naye mahali hapo.
Kijana huyo aliyeonekana kuchoka kimaisha aliitwa Ethan Dylan, alikuwa kijana mwenye asili ya Kingereza ambaye aliishi nchini Marekani. Katika maisha yake yote, hakuwahi kumuona baba yake, kipindi ambacho mama yake aliondoka nchini Marekani na kwenda Uingereza ndipo alipokutana na baba yake, akarudi nchini mwao Marekani ambapo huko ndipo alipokutana na mwanaume aliyeitwa George.
Wawili hao wakapenda na kuoana. George alikuwa mwanaume mpole, aliyejiheshimu ambaye kila siku alitamani sana kumuona Ethan akikulia katika maisha mazuri, yenye heshima ambayo yangemfanya kuwa baba bora miaka ya baadae.
Kutokana na eneo walilokuwa wakiishi kuwa na vijana wengi wenye fujo, waliojihusisha na madawa ya kulevya, naye Ethan akajikuta akiingia katika huo mkumbo na mwisho wa siku kuwa mhuni wa mtaani.
Mama yake aliumia sana lakini hakuwa na cha kufanya. Kama kuongea, aliongea sana lakini hakukuwa na kitu kilichobadilika. Baadaye akajiingiza kwenye makundi ya wahuni, huko akaanza kuuza madawa ya kulevya na mwisho wa siku kumiliki bunduki yake.
Siku hiyo ambayo alizungukwa na watu wengi, alikuwa amemnyooshea bunduki baba yake wa kambo, mzee George. Alimwambia ukweli kwamba alitaka kumpiga risasi. Maneno hayo hayakumshangaza mzee huyo, alichokifanya ni kumsogelea Ethan na kuiweka bunduki ile kwenye paji lake la uso na kumwambia ampige risasi hapohapo.
“Shoot me right here,” (Nipige risasi hapa) alisema mzee George, watu wote waliokuwa wamewazunguka walianza kuogopa kwani walimjua fika Ethan, hakuwa kijana mwenye masihara, alipokuwa akishinda bastola, hakurudisha nyuma hata mara moja, alikuwa tayari kuua, pasipo kutegemea, akaikoki bastola yake kitendo kilichomfanya kila mtu kushtuka mahali hapo. Hata mzee George naye kijasho chembamba kikaanza kumtoka. Ethan alionekana kukasirika mno, hata mwili wake ulimtetemeka.


INAENDELEA...

No comments:

Post a Comment