Friday 26 January 2018

HADITHIIII...........SEHEMU YA SABA

BIASHARA  YA KIFO

SEHEMU YA 7.

 “Ethan, stop,” (Ethan, acha) ilisikika sauti ya mama yake kutoka nyuma.
Ethan hakutaka kuiachia bunduki ile, alikuwa amedhamiria kumuua baba yake wa kambo, hakumpenda kabisa, alimchukia mno, kitendo cha kumuona kila siku katika maisha yake kilimkasirisha.
Alijiandaa kumfyatulia risasi na kumuua kabisa, lakini hata kabla hajafanya hivyo, mama yake akamsogelea na kisha kumzuia kubonyeza kitufe cha bunduki ile. Hiyo ikaonekana kuwa bahati ya mtende kwa mzee George, kwa jinsi alivyomwangalia Ethan, alikuwa amedhamiria kumuua kabisa.
Ethan akaondoka mahali hapo, kundi lile la watu lililokuwa limewazunguka nao wakaondoka kuendelea na kazi zao kama kawaida. 
Hayo ndiyo yalikuwa maisha yake, alichukiwa na kila mtu kwa kuwa alikuwa mtemi, japokuwa alikuwa na miaka kumi na sita lakini tayari Ethan alijifunza maisha ya mitaani hasa ya kutumia bunduki katika maisha yake.
Alikuwa mtu wa fujo, alijulikana sehemu kubwa hapo Manhattan huku akianzisha kundi lake kubwa la kihuni lililojulikana kama The Mobb. Lilikuwa na vijana ishirini, walioshindikana katika maisha yao, walikuwa watumiaji wazuri wa bunduki, walikuwa wavuta bangi na hata wakati mwingine kutumia madawa ya kulevya.
Walikuwa vijana wadogo lakini wale ambao hawakuwa na huruma hata kidogo. Polisi wa hapo Manhattan waliliogopa kundi hili, hawakuyathamini maisha yao, kwao, kupigwa risasi na kufa lilikuwa jambo jema tu kwani waliamini kwamba kulikuwa na mungu wao wa kisela ambaye angewpokea nakuwaingiza katika mbingu yao iliyokuwa na makontena makubwa ya madawa ya kulevya na bangi.
Wakati kundi hilo likiendelea kukua, likiwapiga watu na hata wakati mwingine kuwaua, hapo ndipo walipotumwa polisi waliokuwa na hasira, polisi waliotoka nje ya Manhattan kwa ajili ya kufanya jambo moja tu, kuwakamata vijana hao na hata kama wataleta ubishi au kufanya chochote kilicho kibaya cha kuhatarisha maisha yao, basi wawaue.
Huo ndiyo ulikuwa mwanzo wa kumaliza magenge hayo, vijana wengi walikamatwa na kufungwa gerezani lakini kwa Ethan, akatoroka jijini New York na kuhamia Washington DC ambapo maisha yake yakaendelea.
Hakutaka kuwa mhuni kama alivyokuwa, hakutaka kufanya usela wa mitaani alichokifanya kwa wakati huo ni kujikita katika uuzaji wa madawa ya kulevya kwa kuyasafirisha sehemu moja kwenda nyingine. 
Hapo ndipo alipokutana na wale watu aliokuwa akiwasikia kwamba walikuwa wauzaji wazuri wa madawa ya kulevya na walikuwa watu wenye kuogopwa sana. Alipofikishwa kwa mzee mmoja aliyekuwa na asili ya Mexico, mzee Sanchez El Paso, akamchukua na kumfanya mfanyakazi wake ambaye kazi yake kubwa ilikuwa ni kusafirisha madawa nchini Marekani.
“Ukifanya kazi na mimi, utakuwa tajiri mno,” alisema mzee Sanchez.
“Nitatajirika vipi?”
“Utafahamiana na watu wengi, nisingependa ufanye kazi kwangu milele, pia ningependa baadaye ufanye kazi wewe kama wewe,” alisema mzee Sanchez.
“Ili nifikie ndoto ya kufanya biashara zangu mwenyewe, natakiwa kufanya nini?”
“Kujitoa kazini, hakuna cha zaidi, ila epuka sana wizi, ukiiba na kugundulika, nitakuua,” alisema mzee huyo maneno yaliyomtia hofu mkubwa.
“Siwezi kufanya hivyo! Umenitoa mbali, hakika nitaendelea kukuheshimu na sitokufanyia ujinga,” alisema Ethan.
Alimheshimu mzee huyo kwa kuwa ndiye aliyekuwa akimfanyia mambo mengi na kukutana na watu ambao hakutegemea kukutana nao katika maisha yake. Kila siku alikuwa mtu wa kutoka, hakutulia sehemu moja, leo alikuwa akienda California, kesho Texas na kesho kutwa sehemu nyingine.
Hayo ndiyo yalikuwa maisha yake, kila siku alikuwa akibadilisha muelekeao wake ambapo kote huko kazi kubwa aliyokuwa akiifanya ni kusafirisha madawa ya kulevya tu. Jina lake likaanza kukua, mnyororo mkubwa aliokuwa nao mzee Sanchez ukamsaidia mno na hata katika viwanja vya ndege mbalimbali hakuwa akipata usumbufu wowote ule.
“What do you want?” (Unataka nini?) aliuliza mzee mmoja.
“What do I want? What do you mean?” (Nahitaji nini? Unamanisha nini?)
“For how long have you been doing this work?” (Kwa kipindi gani umekuwa ukifanya kazi hii?)
“Three years?” (Miaka mitatu)
“Ok!” (Sawa)
Alikuwa akizungumza na mzee mmoja aliyekuwa amekaa naye ndani ya ndege. Hakujua ni nani alimwambia kuhusu biashara ya madawa ya kulevya aliyokuwa akiifanya, mzee huyo alianza kumuuliza maswali mengi kiasi kwamba akaanza kuogopa kwani hata humo ndani ya ndege alipokuwemo, alikuwa na mzigo mkubwa aliokuwa akiupeleka Los Angeles.
“Lakini wewe ni nani?” aliuliza Ethan huku akionekana kushikwa na hofu.
“Ninaitwa Boyle Cook,” alijibu mzee yule.
“Umejua vipi kama ninafanya kazi hii?”
“Hauwezi kunificha, ninawajua kwa kuwaangalia, umekuwa na amani katika kufanya kazi hii?” aliuliza bwana Cook.
“Kiasi, si sana, wakati mwingine unakuwa na hofu kubwa.”
“Utakuwa tayari kama nikikupa kazi nyingine, nzuri tu?”
“Kazi gani?”
“Ninataka uwe na amani, siwezi nikakupa kazi ngumu. Niambie, upo tayari?” aliuliza bwana Cook.
“Mmmh!”
“Usijali! Chukua hii, ukiwa tayari niambie,” alisema bwana Cook na kisha kumpa business card yake iliyokuwa na mawasiliano yote.
Mpaka kufikia hatua hiyo Ethan alichanganyikiwa, alikuwa akimwangalia mzee huyo mara mbilimbili, hakumfahamu alikuwa nani, hiyo ilikuwa ni mara ya kwanza kukutana naye, tena walizungumza kwa muda mchache kabla ya mzee huyo kubaki kimya mpaka ndege ilipotua Jijini Los Angeles na kisha kuteremka.
Hawakuzungumza chochote kile, kila mmoja akaendelea na kazi zake zilizomleta ndani ya jiji hilo la starehe. Ethan akaondoka na kupeleka mzigo alipoelekezwa kwani hata kuutoa pale uwanja wa ndege hakukuwa na kazi kubwa kwani kila kitu kiliwekwa tayari.
Kichwa chake kikawa na maswali mengi, alikuwa akijiuliza kuhusu mzee yule ambaye alionekana kumfahamu mno, hakuishia hapo, aliendelea kufikiria hata ile kazi aliyotaka kumpa, hakujua ilikuwa kazi gani ila alimwambia kwamba endapo angekuwa tayari basi amtafute.
Uuzaji wa madawa ya kulevya ilikuwa biashara mbaya na yenye hatari mno lakini hakutaka kuiacha kwani ilimpa kisasi fulani cha fedha na kuanza kuyabadilisha maisha yake. Alichokifanya ni kumpuuzia bwana Cook na yeye kuendelea na maisha yake kama kawaida ingawa mara nyingi mno alikuwa akijiuliza kuhusu mzee yule na kukosa jibu.


INAENDELEA...

No comments:

Post a Comment