Sunday 28 January 2018

HADITHI!III!!!!!!!!!!............SEHEMU YA TISA

BIASHARA YA KIFO
Sehemu ya 09
 Hawakuwa na haja ya gari lile, walikuwa tayari kuliacha lakini wayaokoe maisha yao, hawakutaka kusimama sehemu yoyote ile, waliendelea kusonga mbele kwa kuamini kwamba wangefika sehemu iliyo salama kabisa.

Wakati wamefika umbali urefu, mara wakaanza kuwaona polisi wakiwa mbele yao, tena wakija kwa kasi huku wakiwa na bunduki na mbwa walioonekana kuwa na mafunzo makubwa ya kunusa. Wakati wamebakiza kama hatua mia moja kutoka walipokuwa, wakawaona mbwa wale wakiongeza kasi ya unusaji wao na kuona kwamba iwe isiwe wangeweza kukamatwa.

“Tufanye nini? Turudi tulipotoka au?” aliuliza rafiki yake, Thomson.

“Twende kulia,” alisema Ethan na kuanza kukimbilia upande wa kulia.

Hiyo haikusaidia, mbwa wale waliendelea kuwaongoza polisi kule walipokuwa, tayari waliona kwamba huo ndiyo ungekuwa mwisho wao. Hawakusimama zaidi ya kuongeza kasi zaidi, hiyo wala haikusaidia kwani kadiri walivyoongeza kasi na ndivyo ambavyo polisi wale waliokuwa na mbwa walipozidi kuwafuata, tena nao wakiongeza kasi.

“Wooo...wooo...wooo...” walisikika mbwa wakibweka.

Japokuwa walikimbia sana tena kwa kasi lakini mwisho wa siku wakajikuta wakikamatwa na kutiwa nguvuni. Hawakuwa na jinsi, wakabebwa na kupelekwa Jijini Texas ambapo huko wakafikishwa kituo cha polisi tayari kwa kupelekwa mahakamni.

“Sikutarajia kama kuna siku ningekamatwa,” alisema Ethan.

“Hata mimi! Ila kosa lilikuwa pia?”
“Hatukujipanga, tulikurupuka tu.”

Kesho yake, wakachukuliwa na kupandishwa mahakamani ambapo huko wakajikuta wakikosa dhamana na hivyo kupelekwa rumande. Baada ya wiki mbili Ethan na mwenzake wakarudishwa tena mahakamani ambapo siku hiyo ilionekana kuwa bahati kwao kwani hakukuwa na shahidi yeyote ambaye alijitokeza na kusema kwamba kweli gari hilo liliibwa, hakukuwa na mtu yeyote ambaye alisimama kinyume nao na kuweka ushahidi wao ili wahukumiwe, hivyo mwisho wa siku wakajikuta wameshinda kesi ile.

“Siamini,” alisema Ethan huku akionekana kutokuamini macho yake.

Wakawa huru, Ethan akamuahidi rafiki yake huyo kwamba asingeweza kurudia tabia ya kuiba magari tena kwani kwa kile kilichokuwa kimetokea ni Mungu tu ndiye aliyemsaidia mpaka kuwa huru muda huo. Baada ya kila kitu kuihs amahakamani, wakatoka nje.

“Samahani,” ilisikika sauti ya mwanaume mmoja, alikuwa amemshika bega kwa nyuma, Ethan akageuka.

“Bila samahani.”
“Unahitajika!”

“Wapi? Na nani?”

“Kuna mtu anakusubiri ndani ya gari ile pale.”
“Nani?”
“Twende, utamfahamu tukifika,” alisema mwanaume huyo.

“Twende Thomason....” alimwambia rafiki yake.

“Hapana! Unahitajika peke yako, labda huyu anaweza kusubiri hapa,” alisema mwanaume yule.

Hakuwa na amani kabisa, alikuwa akijiuliza juu ya huyo mtu aliyekuwa akimsubiri ndani ya gari lile. Kwa kuliangalia tu, lilikuwa gari la thamani lililomfanya kuona kwamba mtu aliyekuwa akimiliki gari hilo alikuwa na fedha nyingi.

Hakutaka kusita, alichokifanya ni kuelekea lilipokuwa gari lile, alipolifikia, mlango ukafunguliwa na mwanaume yule kisha kuingia ndani. Kulikuwa na giza, hakukuwa na mwanga, alipokaa kitini, taa zikawashwa na macho yake kutua kwa mwanaume mmoja, hakuwa mgeni machoni mwake, alimfahamu sana, mara ya kwanza kabisa alikutana naye ndani ya ndege na kumpa business card yake, na ndiye yule aliyekuwa akitamani kuwasiliana naye kipindi cha nyuma, alikuwa bwana Boyla Cook.

“Cook!” aliita Ethan kwa mshtuko mkubwa.

“Unaendeleaje Ethan?” aliuliza bwana Cook huku akichia tabasamu pana.”
“Naendelea vizuri, nilikutafuta sana, nilisahau nilipoiweka business card yako, nimefurahi kuonana nawe tena,” alisema Ethan huku akionekana kutokuamini.

“Nimefurahi pia.”

Hapo ndipo bwana Cook alipomwambia kwamba kila kitu kilichoendelea kule mahakamani kilikuwa nyuma yake, alikuwa amepanga kila kitu na ndiyo maana hata mara ya pili alipofikishwa mahakamani pale kesi ilikuwa nyepesi sana kwa kuwa alitumia kiasi kikubwa cha fedha kwa ajili ya kumtoa katika matatizo aliyokuwa nayo.

Ethan akafurahi sana, akamshukuru mzee huyo lakini hapohapo akaanza kujiuliza juu ya msaada ule, mzee yule alikuwa akihitaji nini.

“Nashukuru sana! Ila kwa nini umenisaidia? Na umejuaje kama nilikamatwa?” aliuliza Ethan.

“Nilikuwa nakufuatilia kila kona, nilikwamba kwamba biashara uliyokuwa ukiifanya haikuwa salama kwani muda wowote ule ungekuwa kwenye hatari. Nilitamani sana kufanya kazi na wewe na ndiyo maana kila ulipokuwa, nilihakikisha nakufuatilia kwa ukaribu.

“Wakati mzee Sanchez amefariki, nilitaka kuja kukuchukua lakini nilikuwa na safari ya kwenda Brazil, hivyo nikaamua kuachana nawe kwa muda. Nimerudi siku kadhaa zilizopita na ndipo nilipotuma vijana wakufuatilie na kujua upo wapi, wakasema umekuja huku Texas na umekamatwa kwa kosa la kuiba gari na kutaka kulivusha mpakani, hivyo nikatuma fedha zisaidie kukutoa ili tufanye kazi,” alisema mzee huyo kwa kirefu.

Ethan akashusha pumzi ndefu, hakuamini kile alichokuwa amekisikia, kumbe wakati yeye akijaribu kukumbuka juu ya kile kikaratasi alichokuwa amepewa chenye namba ya bwana Cook, kumbe naye alikuwa akimfuatilia kwa ukaribu. Mpaka kufikia hatua hiyo tayari akajiona kuwa miongoni mwa watu waliokuwa na bahati kubwa.

“Unataka tufanye kazi gani?” aliuliza Ethan.

“Twende nyumbani, tutaongea mengi,” alisema bwana Cook.

“Siwezi kwenda peke yangu, si unajua nina mwenzangu,” alisema Ethan huku akimwangalia rafiki yake, Thomson dirishani.

“Mwambie aje,” aliagiza mzee huyo.

Hapohapo Thomson akaitwa na kisha kuanza safari ya kuelekea nyumbani kwa mzee huyo. Kichwa cha Ethan bado kiliendelea kujiuliza maswali juu ya kazi aliyotakiwa kufanya kwa mzee huyo. Hakuijua ilikuwa ni kazi gani lakini kwa sababu alionyeshewa msaada mkubwa, hakuwa na jinsi, alijiona lingekuwa suala la busara kama angekubaliana naye.

Safari ile ikaishia mbele ya jumba moja la kifahari, kwa kuliangalia wala usingejiuliza maswali kwamba jumba hilo lilikuwa likimilikiwa na mtu mwenye fedha, mtu aliyekuwa na zaidi ya dola bilioni kumi katika akaunti yake. Geti likafunguliwa na kisha gari kuingizwa.

Lilikuwa jumba kubwa lililosheheni vitu vyote ambavyo vilitakiwa kuwa ndani ya jumba la bilionea fulani, kulikuwa na bwana kubwa la kuogelea ambalo sakafu yake ilikuwa ni ya kioo, kulikuwa na mbuga ndogo ya wanyama na kwa mbali kulionekana kuwa na wanyama fulani na ndege wengi, kulikuwa na magari ya kifahari na vitu vingine, ukiachana na hivyo, kulikuwa na masanamu manne ya kike yaliyoonekana kuwa uchi kabisa.

Milango ya gari ikafunguliwa na kisha kuteremka, wakaanza kupiga hatua kuelekea ndani. Muda wote huo Ethan na Thomson walikuwa wakiangalia huku na kule, kila kitu kilichoonekana kwao kilionyesha ni kwa namna gani bwana Cook alikuwa mtu tajiri aliyeogelea fedha.

Walipojingia ndani, kitu cha kwanza kabisa walichokutana nacho ni picha za wanawake wengi zilizokuwa zimebandikwa ukutani, walikuwa watupu kama walivyozaliwa, walikaa katika mapozi tofautitofauti na walikuwa wanawake wa kila asili.

Ethan aliziangalia picha zile, hakuelewa ni kwa nini zilikuwa mahali hapo, ziliusisimua mwili wake kwani kilipita kipindi kirefu hakuwahi kukutana kimwili na mwanamke yeyote yule. Alizunguka huku na kule, macho yake yalikuwa yakiangalia kila kona.

“Mbona kuna picha nyingi sana za wanawake?’ aliuliza Ethan.

“Ninapenda kuwa nazo.”
“Ndiyo ziwe nyingi namna hii?”
“Yeah! Huwa ninafurahia ninapomwangalia mwanamke akiwa mtupu.”
“Mmmh!”

“Ndiyo hivyo! Karibuni sana,” alisema bwana Cook huku akiachia tabasamu pana.

Wakakaa kwenye makochi ya manyoya na kutulia. Wote wawili walikuwa wakiangalia huku na kule, bwana Cook akatoka sebuleni hapo na kuelekea chumbani kwake, baada ya dakika tatu akarudi huku akiwa amebadilisha nguo zake, akaagiza vinywaji, vikaletwa na kuanza kunywa.

“Ninataka unifanyie kazi Ethan,” alisema bwana Cook.

“Kazi gani?”

“Kwanza unajua mimi ni nani?”
“Unaitwa Boyle Cook, sijui kingine zaidi ya hicho,” alijibu Ethan.

“Sawa. Hujawahi kulisikia jina langu sehemu yoyote?”

“Hapana!”

“Mimi ni mkurugenzi wa kampuni ya kutengeneza filamu za utupu ya Bravilian.sex, ni kampuni inayojitegemea na ambayo imetengeneza filamu nyingi mno,” alisema bwana Cook.

“Sawa! Nimefurahi kukufahamu! Kwa hiyo unataka na mimi niigize?”

“Ungependa kuigiza?”
“Hapana! Siwezi kabisa.”
“Sawa! Lengo la kukuita hapa si kutaka uigize bali kuna kazi nyingine nataka uifanye,” alisema bwana Cook.

“Kazi gani?”
“Kunitafutia wasichana wengi duniani kwa ajili ya kuigiza, kila msichana nitakulipa dola elfu kumi,” alisema bwana Cook.

“Mmmh!”

“Ni kazi ngumu?”

“Si sana, kama nitapewa fedha za kutosha kuzunguka duniani, si kazi ngumu, hakuna tatizo,” alisema

“Ila kuna kazi nyingine nataka ufanye, ila kwa siri sana.”
“Kazi ipi?”

“Biashara ya Kifo,” alisema bwana Cook, Ethan na Thomson wakashtuka.

INAENDELEA...                       


No comments:

Post a Comment